USAID KUWANUFAISHA VIJANA WA MIKOA 9 WENYE CHINI YA UMRI WA MIAKA 17




Wakala wa Kimarekani kwa Misaada ya Kimaendeleo ya Kimataifa (USAID) inafadhiri msaada ambao utaanza kuwanufaisha watoto na vijana chini ya umri wa Miaka 17 ambao wataendelea kunufaika na mradi wa “USAID Kizazi Hodari” unaotekelezwa na Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) katika Mikoa tisa (9) na Halmashauri 41 nchini.


Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi Mshiriki anayesimamia matokeo na asasi zinazotekeleza mradi wa “USAID Kizazi Hodari” Kanda ya Kaskazini Mashariki ndg. Aminiel Mongi kwenye kikao cha tathmini ya utekelezaji wa mradi huo Juni 27, 2024 mkoani Shinyanga ambapo pamoja na mambo mengine umelenga kuboresha afya, ustawi na ulinzi wa watoto walio katika mazingira hatarishi pamoja na vijana chini ya Miaka 18 ili kutokomeza maambukizi mapya ya virusi vya UKIMWI.


"Lengo kuu la mradi huu ni kuboresha Afya, ustawi na ulinzi wa watoto waliokatika mazingira hatarishi na vijana kuanzia umri wa Miaka 0 hadi 17 ili kufikia malengo ya kidunia ya kupambana na virusi vya UKIMWI kwa maana wale wenye maambukizi waweze kujua hali zao za maambukizi lakini pia wale ambao wamefahamu hali zao za maambukizi waweze kuunganishwa na vituo vya tiba na mafunzo kwa ajili ya kuanzishiwa dawa, lakini pia wale ambao wameanzishiwa dawa kufika kwenye vituo ili kufubaza maambukizi ya virusi vya UKIMWI”. amesema Mongi

Akizungumza mchumi mkuu idara ya Afya, lishe na ustawi wa jamii kutoka ofisi ya Rais TAMISEMI, ndg. Rashid Kitambulio amesema serikali itaendelea kushirikiana na Kanisa la KKKT katika kufikia malengo yaliyokusudiwa huku akishukuru kwa mradi huo wa USAID kizazi hodari ambao unaendelea kuwanufaisha wahanga hasa wa maambukizi ya virusi vya UKIMWI.


KKKT na mradi wa ‘USAID Kizazi Hodari’ wameitisha mkutano wa wadau wanaoshiriki katika utekelezaji wa mradi huo wakiwemo wawakilishi kutoka Ofisi ya Rais TAMISEMI, Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wanawake na Makundi Maalum, TACAIDS, Kamati ya Usimamizi wa Afya ngazi ya Mikoa na Halmashauri, wadau wanaosimamia afua za tiba na mafunzo katika Mikoa husika lengo ni kupitia na kutathimini utekelezaji wa shughuli za mradi na kuweka mipango endelevu ya mradi huo.


USAID Tanzania kwa ujumla wake inaangazia rasilimali watu kwa afya, mifumo ya taarifa za afya na utumiaji wa data, utawala bora, ufadhili wa afya, ugavi unaotegemewa na sikivu, na ushirikishwaji wa sekta binafsi. Mradi huu unaofadhiliwa na USAID ambao ndio wafadhili wakuu wa mradi huu na mradi unatekelezwa na makao makuu ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) unatekelezwa katika Mikoa tisa (9) ya Tanga, Kilimanjaro, Arusha, Manyara, Singida, Dodoma, Mwanza, Geita na Mara pamoja na jumla ya Halmashauri 41.

Post a Comment

0 Comments